Header Ads Widget

JIMBO LA KIBAJAJI LABADILISHWA JINA, CHILONWA SASA KUITWA CHAMWINO


 Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji (Rufaa) Semistocles Kaijage


TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetangaza kubadilisha majina ya majimbo matatu ya uchaguzi ambapo majimbo yaliyobadilishwa ni Jimbo la Chilonwa ambalo sasa litaitwa Chamwino, Jimbo la Mtera litaitwa Mvumi na Jimbo la Kijito Upele lililopo Mjini Magharibi litaitwa Pangawe.

Kubadilishwa kwa majimbo hayo kunaendelea kufanya idadi ya majimbo ya Uchaguzi kubakia 264 Kama ilivyokuwa katika uchaguzi mkuu uliopita ambapo 214 yapo Tanzania Bara na 50 yapo Zanzibar na kata 3,956.


Pia NEC imetangaza ratiba ya uchukuaji na urejeshaji wa fomu za kugombea Urais katika uchaguzi mkuu ujao kuwa itakua Agosti 5 hadi 25 mwaka huu.


Akizungumza na wandishi wa habari jijini Dodoma leo, Mwenyekiti wa NEC, Jaji Mstaafu Semistocles Kaijage amesema fomu hizo zitatolewa katika Ofisi za Tume hiyo zilizopo eneo la Njedengwa, Dodoma.

Kwa upande wa fomu za Ubunge na Udiwani Jaji Kaijage amesema zitaanza kutolewa kuanzia Agosti 12 hadi 25 mwaka huu na zitapatikana katika Ofisi za Halmashauri na Ofisi za Kata.


"Kwa mujibu Katiba yetu ibara ya 75 inaeleza wazi kuwa Tume inaweza mara kwa mara au angalau baada ya miaka 10 kuchunguza mgawanyo wa Jamhuri katika majimbo, ambapo kupitia ibara hiyo imechunguza na haijagawa majimbo mapya bali imebadilisha majina ya majimbo matatu ambayo nimeyataja," Amesema Jaji Kaijage.