Header Ads Widget

CRDB KANDA YA MAGHARIBI YATOA MSAADA WA VITI NA MEZA 153 SHULE YA SEKONDARI MASUMBWE


Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magaharibi, Said Pamui akimkabidhi Meza Mkuu wa Wilaya ya Mbogwe, Matha Mkupas kama ishara ya kukabidhi madawati 153.

Na Salvatory Ntandu - Mbogwe
Halmashauri ya Wilaya ya  Mbogwe mkoani Geita inakabiliwa na uhaba wa viti na meza  1942 katika shule zake  za sekondari 16 zenye jumla ya wanafunzi  8,975, hali inayosababisha baadhi yao kusoma kwa awamu ili kukabiliana na tatizo hilo.
Kauli hiyo imetolewa Jana Julai 6, 2020 na Mkurugenzi Mtendaji wa  Halmashauri hiyo, Elias Kayandabila katika hafla ya  kupokea viti na meza 153 vilivyotolewa na Benki ya CRDB katika shule ya Sekondari Masumbwe ili kukabiliana na tatizo hilo.
Alisema kuwa shule  hiyo inahudumia kata tatu zilizopo karibu na kata ya Masumbwe ikiwemo Nyakafulu yenye idadi kubwa ya wakazi kutokana na shughuli za uchimbaji ambapo kwa sasa ina viti na meza 1007 na upungufu ni 825 ikilinganishwa na idadi ya wanafunzi ambao ni 1832 sawa na asilimia 45.
“Baada ya Serikali kuanza kutoa elimu msingi bure idadi ya wanafunzi imeongezeka kwa wingi kutokana na jamii za wafugaji kuwa na mwamko wa kuwapeleka watoto shule,” alisema.
Kwa upande wake Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magaharibi, Said Pamui alisema kuwa msaada wa viti na meza walivyotoa vimegharimu Sh Milioni 9,945,000, huku akiwataka wanafunzi kuyatunza ili yaweze kuleta tija sambamba na kupunguza tatizo hilo.
“Nitoe rai kwa wadau wengine nchini kuiga mfano wa CRDB kwa kutoa misaada ya elimu katika halmashauri hii ili kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya tano katika kuwaletea maendeleo wananchi wake kwa kuwapatia huduma nzuri na stahiki,” alisema Pamui.
Akipokea msaada huo, Mkuu wa Wilaya ya Mbogwe, Matha Mkupas alisema kuwa uhitaji wa viti, meza na madawati katika shule za msingi na sekondari bado ni mkubwa na kuwaomba wadau na wazazi kushirikiana na serikali ili kuhakikisha tatizo hilo linapatiwa ufumbuzi wa haraka, huku akiishukuru CRDB kwa kuiunga mkono serikali katika nyanja mbalimbali ikiwemo elimu.
“CRDB ni benki ya kizalendo imekuwa ikitushika mkono katika shughuli mbalimbali za kitaifa tunazozitekeleza katika wilaya hii, niwasihi wananchi, wajasiriamali na watumishi wetu  waendelee kuitumia na sisi kama serikali tutahakikisha tunakuwa pamoja,” alisema Mkupasi.
Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magaharibi, Said Pamui akiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa wilaya ya Mbogwe, Matha Mkupas, Mkurugezi wa Halmashauri ya Mbogwe, Elias Kayandabila na baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari Masumbwe baada ya kukabidhi msaada wa viti na meza shuleni hapo.