` VIONGOZI WA DINI ,SIASA WAUNGANA KUZUNGUMZIA AMANI

WANDAMAN HOTEL

VIONGOZI WA DINI ,SIASA WAUNGANA KUZUNGUMZIA AMANI

Viongozi wa dini, Serikali, na vyama vya siasa nchini wametoa wito kwa Watanzania kudumisha amani, upendo, na mshikamano, huku wakionya dhidi ya matumizi ya majukwaa ya uongozi kuchochea migogoro. 

Katika mfululizo wa hafla za Iftari zilizofanyika mkoani Morogoro na jijini Dar es Salaam, imesisitizwa kuwa umoja wa kitaifa ndio msingi mkuu wa ustawi wa taifa, na ni jukumu la kila kiongozi kutumia ushawishi wake kuwakutanisha wananchi badala ya kuwagawa.

Mkoani Morogoro, Sheikh Rashid Mziwanda, akizungumza katika hafla iliyoandaliwa na Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mussa Kilakala, ameelezea kusikitishwa kwake na baadhi ya viongozi wanaotumia dhamana zao kuhamasisha mivutano. 

Sheikh Mziwanda amesisitiza kuwa ni fedheha kutumia majukwaa ya kiimani au kiserikali kukuza chuki, kwani thamani ya juhudi za binadamu haipo kwenye kile anachokifanya pekee, bali kwenye mwelekeo wa maamuzi sahihi yanayojenga jamii yenye utulivu.

Katika kuitikia wito huo, Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mussa Kilakala, amebainisha kuwa mkutano huo wa kidini ni sehemu ya mkakati wa serikali kuimarisha mahusiano na viongozi wa kiroho ili kulinda utulivu wa mkoa huo. 

Sambamba na hamasa hiyo ya amani, Kilakala ametangaza hatua kubwa za kimaendeleo ambapo Serikali imetoa zaidi ya Shilingi Bilioni 13 kwa ajili ya ujenzi wa stendi ya kisasa katika Kituo cha treni ya mwendo kasi (SGR), hatua itakayorahisisha usafiri na huduma kwa wananchi wanaposhuka kwenye usafiri huo wa kisasa.

Hali kadhalika, jijini Dar es Salaam, Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) kimefanya hafla maalumu katika Ukumbi wa Karimjee iliyowakutanisha viongozi wa vyama mbalimbali vya siasa ikiwemo ACT-Wazalendo, CUF, na CHAUMMA.

Kaimu Msajili wa Vyama vya Siasa, Mohammed Ally Ahmed, amepongeza utamaduni huo wa majadiliano akieleza kuwa historia ya siasa za Tanzania imejengwa katika msingi wa kukosoana kwa staha ili kuboresha mustakabali wa nchi, huku viongozi wengine wakisisitiza kuwa tofauti za kifalsafa majukwaani si uadui, bali ni uhuru wa mawazo unaopaswa kuishia kwenye siasa na kuacha maisha ya kijamii yakiwa na upendo.

Naye Mstahiki Meya wa Manispaa ya Temeke, Uzairu Abdul Athumani, amehitimisha kwa kuwakumbusha wananchi umuhimu wa kusaidiana, hasa katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani. 

Amesema kuwa tendo lolote la wema, liwe dogo au kubwa, lina maana kubwa katika kujenga jamii inayojali wenye uhitaji na watoto yatima, akisisitiza kuwa ushirikiano wa wananchi wenyewe ndio nguzo itakayowanyamazisha wale wote wanaotaka kuchezea utulivu na amani ya Tanzania. 

Kama una Taarifa, Habari, Tangazo n.k Wasiliana nasi kupitia shinyapress@gmail.com au +255 788 469 464