Header Ads Widget

KATAMBI AWATAKA UVCCM SHINYANGA KUACHA SIASA ZA FITINA

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na watu Wenye Ulemavu Patrobas Katambi akizungumza kwenye mkutano wa UVCCM Wilaya ya Shinyanga Mjini.

Na Suzy Luhende, Shinyanga

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na watu Wenye Ulemavu, ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini, Patrobas Katambi ameutaka Umoja wa Vijana (UVCCM) wilaya ya Shinyanga Mjini kuachana na siasa za fitina na kukataa kuyumbishwa, badala yake wawe wakweli na kuweza kutenda haki kwa kila mtu.



Katambi amesema hayo kwenye kikao cha baraza la Umoja wa vijana UVCCM Shinyanga mjini, lililofanyika leo katika ukumbi wa CCM wilaya, ambapo amesema vijana hawatakiwi kujiingiza kwenye kufitinisha wanatakiwa kuwa suluhu ya kila mmoja, ili kuleta maendeleo ndani ya Chama Cha Mapinduzi na kudumisha amani.

"Nawaombeni vijana wenzangu msikubali kushawishika na kuyumbishwa na kufitinishwa kwa ajili ya maslahi ya Chama na mtu yeyote, kwani chama chetu kinasema,fitina kwetu mwiko, hivyo hatutakiwi kukivuruga chama tunatakiwa kukijenga tusiwe na roho mbaya tuwe na upendo wa kweli "amesemma Katambi.

Katambi pia amewataka vijana wote kujisimamia wenyewe na washirikiane kwa pamoja kwa sababu hawagombanii cheo wanagombania majukumu na kutatua kero za wananchi, hivyo wanatakiwa kutetea chama na kulinda amani popote walipo.

"Mimi mwenyewe sitakubali kuyumbishwa na mtu yeyote nitawapigania ,nitasimamia haki kwani inapokuja kwenye maslahi ya Chama hakuna wa kutuyumbisha tunahitaji viongozi bora , kinachotakiwa tumtetee na tumpiganie mwenyekiti wetu wa Chama Cha Mapinduzi CCM Rais Samia Suluhu Hassan",amesema Katambi.

"Mimi hapa ni mdogo sana kwa Chama ila ninawajibika kwa chama na kwa wananchi, cheo ni dhamana maana yake wakati wowote kinachukuliwa na mtu mwingine, hivyo tunatakiwa kufanya kazi kwa kufuata mifumo ya kimaadili ya chama kwa kuwa chama chetu ni chama bora duniani",ameongeza Katambi.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa UVCCM wilaya ya Shinyanga mjini Dotto Joshua amewasisitiza vijana waendelee kufanya kazi kwa bidii na kwa ushirikiano ili kuhakikisha shughuli za chama zinaendelea.

Kwa upande wake Katibu wa Chama Cha Mapinduzi CCM Wilaya ya Shinyanga mjini Ally Majeshi amewataka vijana wasikubali kuwa vibaraka wa watu na kuacha kunong'ona mambo mabaya, kwani wakifanya hivyo yatafika kwenye chombo husika na yatafanyiwa kazi,hivyo wanatakiwa wawe vijana wazuri wapiga kazi na wakubali kukosolewa wanapoonekana wamekosea.

"Kama una changamoto na kiongozi ipeleke kwa siri kwa mhusika mwenyewe usikae kwenye magenge na kuanza kuzungumza changamoto uliyonayo na kiongozi, pia kijana wa CCM hana sifa ya kukaa kwenye genge na kulishwa maneno ya kumtengenezea kashifa kiongozi ama mtu yeyote mjiepushe na watu kama hao tukimgundua kijana wa namna hiyo tunamuondoa", alisema Majeshi.

Majeshi amesema wale viongozi wanaozungumza maneno mabaya vijana wasiyavae na kuyatangaza, kwani wanatakiwa kupita kwenye njia sahihi na kupigania mambo ya Chama wasipiganie mambo ya wengine.

Amewata vijana wakubali kukosolewa pale watakapokosea, pia msikubali kuwa vibaraka wa watu, msijiweke kwenye kundi la mtu, kundi letu liwe la Chama Cha Mapinduzi.

Katibu wa vijana Uvccm wilaya ya Shinyanga mjini Naibu Faraj Katalambula amesema vijana wamejipanga vizuri katika kufanya kazi mbalimbali za Chama na uchaguzi wa chama Cha Mapinduzi CCM.

Katalambula akisoma taarifa kwa niaba ya vijana amesema wanamuomba mbunge wa jimbo hilo Patrobas Katambi awalinde na awapiganie,ambapo na wao wameahidi kumlinda pamoja na wagombea wengine watakaotoka Chama Cha Mapinduzi.

Kwa upande wake mbunge viti maalumu Christina Mzava amewashukuru vijana kwa kazi waliyoifanya katika uchaguzi mkuu wa wabunge na madiwani ambapo pia amewataka waepuke kufanya mambo yasiyo mazuri, hivyo wafanye uchaguzi wa chama kwa staha, wasitafute kubebwa na mtu wafanye wao kama wao.

'Tunataka tuvuke kwa kiwango kikubwa tuangalie masilahi ya chama tusiangalie mambo mengine, tufanye uchaguzi kwa staha,na mnatakiwa kuhamasisha watu wajitokeze wote katika kuandikishwa sensa na makazi itakayofanyika Agosti 23 mwaka huu wasikubali kupotoshwa na baadhi ya watu wasio na malengo mema",amesema Mzava.

Katibu wa CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini All Ally Majeshi akizungumza kwenye mkutano wa UVCCM Wilaya ya Shinyanga Mjini.

Mbunge wa Viti maalum Christina Mzava akitoa neno kwa vijana.

Katibu wa UVCCM Wilaya ya Shinyanga Mjini Naibu Faraji Katalambula akizungumza kwenye mkutano wa UVCCM.


Wajumbe wakiendelea na mkutano.


Mkutano ukiendelea.



Vijana wa hamasa wakitoa burudani

Mbunge viti maalum Christina Mzava


Viongozi wakifuatilia mkutano.

Post a Comment

0 Comments